Dec 1, 2012

Rufaa kusikilizwa na majaji Salum Massati, Katherine Oriyo na Nathalia Kimaro.

RUFAA ya kupinga hukumu ya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam iliyompa ushindi Mbunge wa Ubungo, John Mnyika katika kesi ya uchaguzi dhidi yake, sasa imeiva.
Tayari rufaa hiyo imeshapangiwa jopo la majaji watu wa Mahakama ya Rufani watakaoisikiliza na kuitolea uamuzi na imepangwa kusikilizwa wiki ijayo.
Kwa mujibu wa ratiba ya vikao vya Mahakama ya Rufani, rufaa hiyo imepangwa kusikilizwa Desemba 7 mwaka huu.
Ratiba hiyo inaonyesha kuwa rufaa hiyo itasikilizwa na majaji Salum Massati, Katherine Oriyo na Nathalia Kimaro.
Rufaa hiyo ilifunguliwa Oktoba 25 mwaka huu na aliyekuwa mgombea wa ubunge katika Jimbo la Ubungo kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Hawa Ng’humbi, aliyekuwa mlalamikaji katika kesi ya msingi.
Mahakama Kuu katika hukumu yake iliyotolewa na Jaji Upendo Msuya Mei 24, 2012, ilitupilia mbali madai ya Ng’humbi ikisema alishindwa kuyathibitisha na badala yake, ikamthibitisha rasmi Mnyika kuwa mbunge halali wa jimbo hilo. Hata hivyo, Ng’humbi hakukubaliana na hukumu hiyo, ndipo akakata rufaa akiiomba hukumu hiyo itenguliwe.
Ng’humbi anayewakilishwa na Wakili Issa Maige, katika rufaa yake hiyo ameorodhesha hoja 10 za kupinga hukumu hiyo, akidokeza kile anachokiona kuwa ni udhaifu katika hukumu hiyo.
Pamoja na mambo mengine, Ng’humbi anadai kuwa Jaji aliyesikiliza kesi ya msingi na kutoa hukumu hiyo, alikosea katika kutafsiri sheria na kupima ushahidi wa pande zote.
Ng’humbi anadai kuwa jaji alikosea kisheria na kiukweli kwa kusema kuwa makosa yaliyobainika katika ujumlishaji na kuhesabu kura na kusababisha kuwapo kwa kura 14,854, zisizohesabiwa hayakuathiri matokeo ya uchaguzi.
Anadai kuwa aliweza kuthibitsha kuwapo kwa makosa katika mchakato wa uchaguzi yaliyosababisha kuwapo kwa kura 14, 854 zisizohesabiwa na kwamba jaji alikosea kisheria na kiukweli kwa kutokuhamishia kwa mdaiwa, jukumu la kuelezea sababu za kuwapo kwa dosari hizo.
“Jaji alikosea kisheria na kiukweli kusema kwamba kura 14,854, ambazo hazikuhesabiwa zilitokana na makosa ya kibinadamu, bila kuwepo na ushahidi kuhusu hilo katika kumbukumbu za mahakama.”
Katika hoja nyingine, Ng’humbi anadai kuwa jaji alikosea kisheria na kiukweli kwa kusema kuwa hazikutumika kompyuta ambazo hazikuwa zimeidhinishwa na mamlaka husika katika kujumlisha na kura.

No comments: