![](https://lh3.googleusercontent.com/blogger_img_proxy/AEn0k_tUZztqwnyY3fHbRDR-KAUjiWGhUlFN3lLU0d60X24mRYWCVAkI-gqKYutYDy3iCMkX-bZ2Zyr6WzD5S-k3xODs626z5-2Q9rZbLU0Jcpf0udDWqV8fSLQ0fueZxRUPTvUyJnXgJRWXpeSsgfII5JRwElJVCSKsR48lwCed_4Xder5GkpSJ=s0-d)
Fundi wa Kampuni ya Reli Tanzania (TRL), akiwa akirabati reli katika Makutano ya Barabara za Mandela na reli hiyo, eneo la Tabata Relini jijini Dar es Salaam jana, kabla ya kuanza rasmi kwa usafiri wa reli keshokutwa.Picha na Rafael Lubava
Hatimaye usafiri wa treni katika Jiji la Dar es Salaam, utaanza rasmi keshokutwa baada ya maandalizi yote kukamilika.
Kuanza kwa usafiri huo, ni utekelezaji wa ahadi ya Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, katika kikao cha Bunge cha bajeti ambapo alisema usafiri huo ungeanza Oktoba mwaka huu.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Naibu Waziri wa Uchukuzi, Dk Charles Tizeba, alisema maandalizi yote yamekamilika na usafiri utaanza Jumatatu.
Alisema usafiri huo utakaoendeshwa na Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (Tazara) na Kampuni ya Reli Tanzania (TRL) utakuwa ukianza saa 11.00 alfajiri hadi saa 2.00 usiku.
“ Treni zitakuwa zikipumzika kuanzia saa 5.00 asubuhi hadi saa 9.00 jioni,” alisema Dk Tizeba.
Alisema kwa treni ya Tazara itakayokuwa itanzia Dar es Salaam hadi Mwakanga nauli yake itakuwa Sh500 kwa mtu mzima na Sh 100 kwa mtoto na wanafunzi.
Dk Tizeba alisema kwa treni ya TRL, itakayoanzia katikati ya Jiji hadi Ubungo Maziwa, nauli itakuwa Sh400 kwa mtu mzima na wanafunzi watatozwa Sh100.
Alisema abiria watatakiwa kununua tiketi kabla ya kupanda treni ambazo watazionyesha mlangoni wakati wanaingia.
“Tuna vituo zaidi ya 2,000 vya wauza tiketi ambao wengine watakuwa kwenye vituo vya kupandia treni wakiziuza, zitapatikana kwa urahisi kama ilivyo kwa vocha za simu za mkononi,” alisema Tizeba.
Alisema wataanza na treni moja kwa Tazara na nyingine kwa TRL ambazo zitakuwa zikienda na kurudi, lakini baadaye zitaongezwa ili ziwe zinapishana katika kila njia.
Alisema uzinduzi mdogo utafanyika Ubungo Maziwa na Tazara Jumatatu kuanzia saa 12.00 asubuhi na kwamba kazi hiyo itafanywa na Waziri wa Uchukuzi, Dk Mwakyembe.
“Uzinduzi kamili utafanywa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda katika siku itakayopangwa baadaye,” alisema Dk Tizeba.